Friday, January 18, 2019

Tabia 5 zinazokufanya usikubalike katika jamii.

Tabia 5 zinazokufanya usikubalike katika jamii.
Je, umewahi kujiuliza kwa nini mtu inatokea hakubaliki kwenye jamii? Akitokea kama watu walikuwa wakizungumza, huacha. Kila anachozungumza wengine wanapinga nk.

Zipo sababu kadhaa ambazo zinaweza kufanya mtu asikubalike. Lakini hapa kwenye mada yetu nitakupa sababu tano kubwa zaidi, ambazo zimebeba nyingine nyingi ndani yake.

1. UBABE KUPITILIZA
Siyo jambo zuri mtu kuwa mpole kupitiliza kiasi cha kuonewa na kila mtu. Lakini haitakiwi kuwa mbabe kupitiliza. Mbabe hana nafasi ya kukubalika kwenye jamii. Ubabe ni pamoja na kuwaonea wengine au kuwapiga kwa maneno au nguvu.

Kuna ubabe wa kukataa hoja kwenye vikao au kuwatusi wengine ambao wapo chini yake. Ukiwa na tabia hii tegemea kutokubalika kwenye jamii yako.

2. MARINGO
Maringo ni tabia nyingine mbaya ambayo husababisha kwa kiasi kikubwa usikubalike. Ukionyesha maringo kupitiliza hakuna mtu atakayependa kuwa karibu nawe, maana ni moja ya viashiria vya dharau na majivuno.

Mtu anayeringa hana rafiki na taratibu atajikuta akigombana na kila mtu na baadaye atajikuta anaishi kwenye dunia ya peke yake.

3. MASENGENYO
Kusengenya wengine ni tabia isiyokubalika na jamii. Kwa bahati mbaya sana ni kwamba, msengenyeji huwa hajui kama ana tabia hiyo.

Ilivyo ni kwamba, mtu anayesengenya wengine hujisahau. Leo akiwa mahali anamsema fulani, kesho atakwenda kuzungumza na yule aliyemsengenya jana, akimsengenya mwingine.

Taarifa za usengenyaji zikisambaa, mwishowe anajikuta akiwa hakubaliki tena na watu wanaomzunguka. Anashangaa ghafla anaishi kwenye dunia ya peke yake. Hakuna anayemkubali.

Akitokea mahali, wenzake wanainuka na kumuacha peke yake. Alama hii ikuzindue usingizini na ukae mbali na usengenyaji ili usijitengenezee mazingira ya kutokubalika kwenye jamii unayoishi.

4. KUTOJITOA
Kuna watu wana tabia za ajabu sana… yanapotokea mambo kwenye jamii hana muda wa kushiriki. Hili ni tatizo kubwa na husababisha watu wakutenge. Leo amepelekewa kadi ya harusi, hachangi.

Unatokea msiba jirani yake, haendi na hatoi rambirambi. Sawa… mwingine anaweza kutoa rambirambi, lakini msibani hafiki. Hilo ni tatizo. Jamii itakuhesabu kama sehemu yake ikiwa utashirikiana nao kwa karibu kwenye kila kitu.

Kujifanya bize sana hakuna maana. Ili ufahamu madhara ya jambo hili ni pale ambapo utapwa na tatizo. Mfano unaweza kuugua hadi kufikia kulazwa, ukashangaa hakuna mtu anayekuja kukutembelea na kukupa pole, ujue kuna tatizo.

Mwingine inatokea anafiwa, watu wanasusa kufika msibani. Kama wakifika basi hutenda kama unavyotenda. Watatoa michango yao kisha watakuambia wana kazi za kufanya, wataondoka.

Kimsingi binadamu ni rahisi kukuonyesha ulivyo kwa kupitia wao wenyewe. Kwa maana hiyo kama una tabia hiyo, watakulipizia kwa namna ileile ili nawe ikuume kwa staili ileile.

5. HOFU YA MUNGU
Binadamu ambaye anaonekana hana hofu ya Mungu, hana rafiki. Wapo baadhi ya watu hawazingatii imani zao, hawana ubinadamu na mara kadhaa wameonyesha wazi namna ambavyo hawana hofu kufanya mambo mabaya ambayo mwenye imani na hofu ya Mungu hawezi kufanya.

Mtu asiye na hofu ya Mungu hufanya mambo ya hovyo mbele za jamii, yasiyo na nidhamu au utu bila kujali. Hakuna mtu ambaye atapenda kuwa karibu na mtu wa aina hiyo.

TENGENEZA KUKUBALIKA
Usisubiri yote hayo yakukute wakati tayari umeshagundua namna ya kukufanya ukubalike. Ikiwa una moja ya tabia nilizotaja hapo juu, tafadhali badilika.

Lakini hata kama huna tabia hizo, angalau utakuwa umeshaujua ukweli ulivyo na utakuwa makini kujiweka mbali na tabia za namna hiyo.